Welcome to VIVAX MEDIA, feel free to Comment and dont forget to Share (also please Click on the YOUTUBE, YOUTUBE, YOUTUBE button above/bellow the page).....!! Welcome to VIVAX MEDIA, feel free to Comment and dont forget to Share (also please Click on the YOUTUBE, YOUTUBE, YOUTUBE button above/bellow the page).....!! Welcome to VIVAX MEDIA, feel free to Comment., dont forget to Share (also please Click on the YOUTUBE, YOUTUBE, YOUTUBE button above/bellow the page).....!! Welcome to VIVAX MEDIA, feel free to Comment., dont forget to Share (also please Click on the YOUTUBE, YOUTUBE, YOUTUBE button above/bellow the page).....!!

ZIFAHAMU NJIA ZA UZAZI WA MPANGO.

ZIFAHAMU NJIA ZA UZAZI WA MPANGO:;        

            Njia za uzazi wa mpango hutumika na wanaume na wanawake kuzuia ujauzito kwa madhumuni ya kupanga uzazi ili kuwa na familia bora. Ni vigumu kusema kuwa kuna njia iliyo bora zaidi ya uzazi wa mpango kwa kuwa kila njia ina faida na hasara zake. Wote kati ya mwanamke na mwanaume wana maamuzi juu ya mipangilio wa kupata watoto.


Kufanya uchaguzi utumie njia ipi kwa ajili ya kupanga uzazi siyo kitu rahisi kwa kuwa kuna mambo mengi ya kuzingatia kabla ya kufanya maamuzi yeyote. Lakini awali kabisa, inabidi
ujifunze njia mbali mbali, ili kuweza kubaini ni njia ipi itakayokufaa pamoja na mwenzi wako kupanga uzazi. Mnaweza pia kuwasiliana na muuguzi au daktari anayeusiana na masuala ya uzazi wa mpango kwa ushauri, ili muweze kuchagua njia sahihi itakayowafaa.
Kabla ya kutumia njia yeyote ya uzazi wa mpango, inabidi ufikirie kuhusu mambo yafuatayo:
  • Afya yako kwa ujumla.
  • Ni kwa kiwango gani njia husika ya uzazi wa mpango inafanya kazi.
  • Unajamiiana mara ngapi?
  • Matarajio ya kupata mtoto siku za usoni.
  • Je ni nini faida na madhara ya kutumia njia husika ya uzazi wa mpango?
  • Je unafurahia kutumia njia husika uliyochagua?

Yakupasa kufahamu kuwa, hata kama njia unayotumia ni bora zaidi, wakati mwingine njia hiyo yaweza kushindwa kufanya kazi. Lakini uwezekano wa kupata ujauzito utakuwa mdogo sana endapo njia uliyochagua itatumika kwa usahihi wakati wa kujamiiana. Pia ikumbukwe pia, njia za uzazi wa mpango za kutumia homoni na dawa, hazitakukinga na maambukizi ya HIV na magonjwa ya zinaa.
Zifuatazo ni njia mbali mbali ambazo zaweza kutumika kwa ajili ya uzazi wa mpango na jinsi zinavyofanya kazi. Njia mojawapo ni njia ya asili ya kutumia kalenda.Kuifahamu zaidi njia hii tembelea ukurasa wetu wa AFYA YA MAMA NA MTOTO katika mtandao huu.
Njia nyingine ni ya dawa mseto za vidonge vya kumeza. Vidonge hivi vina homoni za kutengeneza za estrogen na progestin. Dawa za vidonge vya uzazi wa mpango hufanya kazi kwa kuzuia kutolewa kwa mayai kutoka katika ovari. Njia nyingine ya ufanyaji kazi wa dawa hizi ni kuufanya ute ulio katika mlango wa uzazi kuwa mzito kiasi kwamba huzuia mbegu za kiume kuogelea kulekea katika tumbo la uzazi na kuzuia urutubishaji wa yai.
Huwa kuna aina tofauti za dawa za vidonge vya uzazi wa mpango.Ni vyema ukawasiliana na daktari wako ili kuweza kufahamu ni dawa gani itakayokufaa. Daktari wako anaweza kukushauri kutokutumia dawa hizi kama:
  • Una tatizo la kuganda kwa damu katika mishipa ya damu.
  • Umewahi kupata au una kansa ya matiti, kansa ya ini au kansa ya kizazi.
  •  Kama ni mwanamama mwenye miaka zaidi ya 35 na unavuta sigara.
  • Kama unatumia aina fulani ya dawa za antibiotiki.

 Dawa za antibiotiki zaweza kupunguza uwezo wa ufanyaji kazi wa dawa za uzazi wa mpango, na mwanama anaweza kupata ujauzito. Zungumza na mfamasia wako na daktari ili uweze kutumia njia mbadala endapo utakua unatumia antibiotiki.
Plasta ya kubandika ni njia nyingine ambayo hutumika kama dawa za uzazi wa mpango. Plasta hii hubandikwa katika ngozi chini kidogo ya tumbo, kwenye mkono au paja na sehemu ya  juu ya mwili kama kifuani. Plasta hii hutoa homoni ya estrogen na progestrin na husharabiwa katika mfumo wa damu. Dawa hii hufanya kazi kama ilivyo ya vidonge kwa kuzuia upevushaji wa yai katika ovari. Pia huufanya ute wa mlango wa uzazi kuwa mzito na kuzuia mbegu za kiume kupita kwenda kurutubisha yai. Kibandiko hiki cha plasta hutumika mara moja wiki na kwa wiki tatu kila mwezi. Wiki ya nne mwanamama hatotumia kibandiko hiki ili aweze kupata siku za hedhi kwenye mzunguko huo.
Dawa za kuchoma katika misuli na husharabiwa kwenye mishipa ya damu kwa njia ya sindano kama Depo Provera®. Mwanamama anayetumia njia hii huchomwa  sindano ya homoni ya progestrin katika mkono kila baada ya miezi mitatu. Njia hii pia huzuia upevushaji wa yai kutoka katika ovari na kuufanya ute wa njia ya uzazi kuwa mzito na kuzuia mbegu za kiume. Dawa hii isitumike zaidi ya miaka miwili kwa kuwa yaweza kusababisha tatizo la mifupa ambalo huisha baada ya kuacha. Endapo itatumika kwa muda mrefu zaidi ya hapo yaweza kusababisha udhaifu wa mifupa (kitaalam kama osteoporosis).
Ringi ya kuweka  kwenye uke ni njia nyingine ambayo hutoa homoni za estrogen na progestrin. Na hii vile vile hufanya kazi kwa kuzuia upevushaji wa yai katika ovari na huufanya ute wa njia ya mlango wa uzazi kuwa mzito na kuzuia mbegu za kiume kupita. Mwanama huibinya ringi katikati kwa kutumia
kidole gumba na cha shahada na kuingiza ndani ya uke. Ringi hii huvaliwa kwa wiki tatu na hutolewa mwanamama anapoona siku zake za hedhi na hutumia ringi mpya katika mzunguko unaofuata.
Kipandikizi(kijiti) ni aina ya kifaa chenye ukubwa wa kadiri ya njiti ya kiberiti, hujikunja kwa urahisi na huwekwa chini ya ngozi kwenye sehemu ya juu ya mkono. Kipandikizi hutoa homoni ya progestrin ambayo hubadilisha hali ya ukuta wa uzazi na pia kuufanya ute wa njia ya uzazi kuwa mzito na kuzuia yai kurutubishwa.Njia hii huweza kufanya kazi kwa muda wa miaka mitatu.Muuguzi au daktari atamsaidia mwanamama kuweka kipandikizi.
Kipandikizi cha kwenye tumbo la uzazi(intrauterine devices-IUD), chenye umbo la herufi “T”, Kifaa hiki kidogo huwekwa katika tumbo la uzazi na kuna aina mbili za kifaa hiki:
  • Kipandikizi cha shaba(Copper IUD),kifaa hiki hufanya kazi kwa kutoa kiasi kidogo cha madini ya shaba katika tumbo la uzazi na kuzuia mbegu za kiume kurutubisha yai, kama yai litarutubishwa madini haya yatazuia yai hilo lisipandikizwe katika ukuta wa uzazi. Mwanamama atahitaji usaidizi wa daktari katika uwekaji wa kifaa hiki. Kifaa hiki chaweza kubaki kikiendelea kufanya kazi kwa muda wa miaka mitano hadi kumi.
  • Kipandikizi chenye homoni (Hormonal IUD) kifaa hiki ambacho hupatika kwa jina la Mirena®, hutoa homoni ya progestrin katika tumbo la uzazi na kuzuia upevushaji wa yai pamoja na kuufanya ute wa njia ya kizazi kuwa mzito na kuzuia urutubishaji. Huzuia pia yai lililorutubishwa kupandikizwa  katika ukuta wa uzazi. Usaidizi wa daktari huitajika katika uwekaji wa kifaa hiki ambacho hudumu hadi kufikia miaka mitano.

Baada ya kujifungua mwanamama apate ushauri wa daktari kabla ya kutumia dawa za uzazi wa mpango zenye homoni za estrogen na progestrin. Dawa hizi zaweza kuongeza hatari ya kuganda kwa damu, tatizo ambalo hujitokeza baada ya kujifungua. Wakinamama waliojifungua kwa njia ya upasuaji au wana matatizo yanayoweza kusababisha kuganda kwa damu, uzito mkubwa, historia ya damu kuganda, wanavuta sigara, au kifafa cha mimba wanahitajika kusubiri angalau kwa wiki sita, hii ni baada ya kujifungua.
Kufunga uzazi kwa njia ya kipandikizi (sterilization implant),hii ni njia ya kufunga uzazi bila upasuaji kwa kinamama. Huu ni mrija mwemba ambao hutumika kuingiza koili ndogo kwenye kizazi hadi kufikia mirija ya kupitisha mayai (fallopian tubes).Kifaa hiki hufanya kazi kwa kusabisha tishu za kovu kutengenezwa katika mirija ya uzazi na kuziba njia ya kupitisha mayai. Kutengenezwa kwa kovu huchukua muda wa miezi mitatu, kwa hiyo katika kipindi hicho, mwanamama hushauriwa kutumia njia nyingine za uzazi wa mpango. Baada ya miezi mitatu mwanamama hutakiwa kwenda hospitali kuchunguzwa kama kovu lilijitengeneza na kuziba kabisa mirija ya kupitisha mayai.
Kufunga uzazi kwa njia ya upasuaji (surgical sterilization), kwa njia hii upasuaji hufanyika na kufunga mirija ya kupitishia mayai aidha kwa kuikata mirija, kuifunga au kuiziba.Hii huzuia mayai kupitishwa kwenda kwenye tumbo la uzazi. Upasuaji huu pia waweza kufanywa mwanamama anapojifungua kwa njia ya upasuaji ili kuepusha upasuaji mwingine.
Njia hii kwa wanaume hujulikana kama vasectomy, ambapo kwa kuikata au kuifunga mirija ya kupitisha mbegu za kiume hufanya mwanaume kutoa maji maji yasiyo na mbegu hizi na hivyo kutokuwa na uwezo wa kumpa mimba mwanamke. Mbegu za kiume zaweza kubaki katika mfumo wa uzazi wa mwanaume kwa miezi mitatu baada ya upasuaji, kwa hiyo njia nyingine za uzazi wa mpango hazina budi kutumika ili kujikinga na ujauzito usiotarajiwa. Baada ya muda huo utafiti mdogo hufanyika kuhakiki uwepo wa mbegu hizo.                             Katika sehemu ya kwanza tuliona uchaguzi kufahamu utumie njia ipi kwa ajili ya kupanga uzazi.Uchaguzi wa njia hizi siyo kitu rahisi kwa kuwa kuna mambo mengi ya kuzingatia kabla ya kufanya maamuzi yeyote. Lakini awali kabisa, inabidi ujifunze njia mbali mbali, ili kuweza kubaini ni njia ipi itakayokufaa pamoja na mwenzi wako kupanga uzazi. Mnaweza pia kuwasiliana na muuguzi au daktari anayeusiana na masuala ya uzazi wa mpango kwa ushauri, ili muweze kuchagua njia sahihi itakayowafaa.Pia tulijifunza kuhusu njia mbali mbali tukiangalia faida na hasara zake.Zifuatazo ni njia nyinginezo
ambazo zaweza pia kutumika kupanga uzazi. Njia hizi ni kama njia ya dharura na njia za vizuizi.
Njia ya dharura za uzazi wa mpango huusisha matumizi ya dawa za kumeza(morning after pills). Njia hii humsaidia mwanamama asipate ujauzito endapo atajamiiana bila kutumia njia yeyote, au pengine njia aliyoitumia kwa ajili ya kupanga uzazi haikutumika kwa usahihi au haikufanya kazi (mfano kupasuka kwa mpira wa kiume). Kuna wakati pia mwanamama anaweza kusahau kumeza vidonge vya uzazi wa mpango.
Njia hii ya dharura imekuwa muhimu sana kwa watoto wa kike na kinamama wanaotendewa ukatili kwa kubakwa au kushawishiwa kushiriki katika vitendo vya ngono na watu wenye hila mbaya.
Dawa za dharura za uzazi wa mpango hutumiwa katika dozi moja au dozi mbili. Dawa iliyo na dozi moja hufanya kazi sawa na ile iliyo na dozi mbili. Dawa hii ya homoni hufanya kazi kwa kuzuia upevushaji wa yai katika ovari au kuzuia mbegu za kiume (sperm) kurutubisha yai. Dawa hii hutumika kabla ya saa 72 kupita baada ya mwanamama kujamiaana bila kutumia njia yeyote kupanga uzazi.
Vizuizi ni aina nyingine za njia za uzazi wa mpango ambazo haziusishi matumizi ya dawa za homoni .Njia mojawapo hujulikana kama kiwambo (diaphragm). Kiwambo hiki hutengenezwa kwa  kutumia mpira na chenye umbo la bakuli ndogo. Kiwambo hiki hupatikana katika ukubwa tofauti, na mwanamama atahitaji msaada wa daktari ili aweze kufahamu ukubwa wa kiwambo kitakachomfaa. Uwekaji wake hautahitaji msaada wa daktari kama ilivyo kwa vipandikizi.
Kabla ya kujamiaana mwanamama hukiweka kiwambo kufunika mlango wa kizazi (cervix). Kiwambo hufanya kazi kwa kuzuia mbegu za kiume kuogelea kuelekea tumbo la uzazi na huitaji kuondolewa ndani ya muda wa saa 24.
Mipira ya kike(female condom), ni aina nyingine ya kizuizi, ambayo huvaliwa na mwanamama katika uke. Njia hii hufanya kazi kwa kuzuia mbegu za kiume kuingia katika tumbo la uzazi.Aina hii ambayo hutengenezwa kwa mpira mwembamba ina ringi mbili.Ringi ya ndani(iliyo ndogo) ambayo huingizwa na kujishika kwa ndani na ringi ya nje(iliyo kubwa) huzuia sehemu ya nje ya mpira kuingia ndani ya uke wakati wa kujamiiana. Mpira huu waweza kuvaliwa masaa 8 kabla ya kujamiina na humpa uhuru zaidi mwanamama katika maamuzi ya kutumia mpira ukilinganisha na mipira ya kiume. Mpira utahitajika kubadilishwa endapo mwanamama atajamiiana tena. Mpira huu usitumike pamoja na mpira wa kiume kwa wakati mmoja.
Mpira wa kiume(male condom), huvaliwa kwenye uume baada ya kuhemka.Aina hii ya kizuizi hutengenezwa kwa mpira (latex,polyurethane).Kila wakati mwanaume anapojamiaana huitaji kubadilisha mpira mpya.
Ili isipoteze ubora wake mipira ya kiume na kike inahitaji kuhifadhiwa sehemu kavu na isiyo na joto. Epuka kutumia vilainishi vya mafuta kwa kuwa huaribu mpira na waweza kupasuka.Vilainishi kama gel zinazochanganyika na maji zaweza kutumika mfano K-Y Gel®.
Je njia zote za uzazi wa mpango zaweza kuzuia HIV na magonjwa ya zinaa?
Jibu ni hapana. Mpira wa kiume ndiyo njia pekee iliyofanyiwa utafiti na kuonekana kuwa na uwezo wa kukinga magonjwa ya zinaa na HIV ingawa siyo kwa asilimia mia moja. Tafiti zinaendelea kuchunguza  mipira ya kike kama yaweza kuzuia maambukizi ya HIV na magonjwa ya zinaa.
Share And Comment Bellow On What You Think About This Post!!!

Comments

Facebook Twitter Youtube