Welcome to VIVAX MEDIA, feel free to Comment and dont forget to Share (also please Click on the YOUTUBE, YOUTUBE, YOUTUBE button above/bellow the page).....!! Welcome to VIVAX MEDIA, feel free to Comment and dont forget to Share (also please Click on the YOUTUBE, YOUTUBE, YOUTUBE button above/bellow the page).....!! Welcome to VIVAX MEDIA, feel free to Comment., dont forget to Share (also please Click on the YOUTUBE, YOUTUBE, YOUTUBE button above/bellow the page).....!! Welcome to VIVAX MEDIA, feel free to Comment., dont forget to Share (also please Click on the YOUTUBE, YOUTUBE, YOUTUBE button above/bellow the page).....!!

Akina mama waajiriwa washauriwa kunyonyesha watoto ipasavyo

    
SIYO kwamba sijui faida za maziwa ya mama kwa mtoto.
Nafahamu wazi kwamba, maziwa ya mama ndiyo chakula pekee kinachompatia mtoto virutubisho (viini lishe) vyote muhimu anavyohitaji kwa uwiano ulio sahihi kwa ajili ya ukuaji na maendeleo yake. Nafahamu kabisa kwamba, maziwa ya mama humpatia mtoto kinga dhidi ya maradhi mbalimbali kama vile kuharisha, magonjwa ya njia ya hewa na masikio. Lakini pia humwezesha mtoto kukua kimwili na kiakili kikamilifu. Zaidi ya yote, ninazo taarifa za kitaalamu kwamba, unyonyeshaji huleta uhusiano mzuri na wa karibu kati ya mama na mtoto.
Kupitia machapisho mbalimbali na hata mafunzo ya moja kwa moja ya wataalamu, naelewa kwamba watoto walionyonya maziwa ya mama huwa na mwenendo mzuri pamoja na akili ukilinganisha na wale wasionyonya maziwa ya mama. Hata kwenye kliniki ya ujauzito, wauguzi na wakunga wamenielewesha kuwa maziwa ya mama humeng’enywa (huyeyushwa) kwa urahisi tumboni mwa mtoto na hivyo kutumiwa na mwili kwa ufanisi.
Ikiachwa faida kwa mtoto, ninayo maarifa kwamba unyonyeshaji pia husaidia kulinda afya ya mama. Nimesoma hata kwenye machapisho ya afya kwamba, mama anaponyonyesha mara baada ya kujifungua husaidia tumbo la uzazi kurudi katika hali ya kawaida mapema. Pia husaidia kupunguza damu kutoka hivyo kuzuia upungufu wa wekundu wa damu (upungufu wa damu). Jambo lingine ambalo mimi na akina mama wengi tunalifahamu hata bila msaada wa wataalamu, ni kwamba unyonyeshaji hupunguza uwezekano wa kupata ujauzito.
Ni endapo mama atamnyonyesha mtoto katika miezi sita ya maziwa yake tu, mara nyingi kwa siku na pia kama hajapata hedhi; Mafunzo mengine ambayo nimeyapata kwa njia tofauti, ni kwamba, kumnyonyesha mtoto hupunguza uwezekano wa kupata saratani ya mfuko wa uzazi, na matiti. Pamoja na faida hizo kwa mama na mtoto, baada ya kujifungua watoto pacha, sikufanikisha kuwanyonyesha kama ambavyo kanuni zinaelekeza. Sikuwa na namna ya kuwalazimisha wanangu wanyonye; kwani walinigomea wakiwa na miezi sita.
Hawakutaka kuendelea kunyonya maziwa yangu. Tatizo lilianza wakiwa na miezi mitano. Walinogewa na maziwa ya kopo. Hii ni kwa sababu baada ya kumaliza likizo yangu ya uzazi ya miezi mitatu na kuanza kazi, ilinilazimu kuwaanzishia maziwa mbadala. Kutokana na msongamano wa barabarani katika jiji la Dar es Salaam, nilikuwa nikifika jioni nyumbani na kukuta wameshakunywa maziwa ya kopo. Kwa hiyo walizoea maziwa hayo ya kopo ambayo naamini yaliwafanya wapoteze hamu ya maziwa yangu.
Isitoshe, nionavyo, maziwa ya kwenye chupa yalitoka kwa wingi ikilinganishwa na ya mama ambayo yalitoka kidogo. Hayakuwatosheleza watoto hao pacha. Sikuwa na njia nyingine ya kuwatosheleza watoto zaidi ya kuingia mfukoni kwa ajili ya kununua maziwa ya kopo na vyakula vingine vya kuwawesha kuwaongezea lishe mwilini. Lakini pia nakumbuka, ile kanuni ya kwamba, mtoto aanze kunyonya maziwa ya mama mara tu baada ya kuzaliwa (katika saa moja ya kwanza), kwangu haikufanyika.
Kuchelewa kunyonyesha baada ya kujifungua
Baada ya kujifungua kwa operesheni, ilinichukua saa nyingi kabla ya watoto kuletwa niwanyonyeshe maziwa ya kwanza. Lakini haikuwezekana kutokana na kwamba, maziwa yalikuwa hayatoki. Tatizo la kuchelewa kuanza kuwanyonyesha kwa wakati watoto mara nyingi huwapata wazazi wanaojifungua kwa operesheni, lakini wakati mwingine huchangiwa na wauguzi wasio makini.
Kwa ujumla, sikutimiza maelekezo ya kitaalamu yanayotaka mtoto asipewe kitu kingine chochote hata maji, isipokuwa maziwa ya mama mpaka afikie umri wa miezi sita. Kwani wanangu walianza kupewa uji na maziwa ya kopo wakiwa na umri wa miezi mitatu. Hiyo ni simulizi ya Shukuru Amani (siyo jina halisi) alipofanya mahojiano na waandishi wa makala haya. Shukuru anawakilisha kilio cha wanawake wengi ambao mazingira, hususani ya ajira, yamewafanya washindwe kuwanyonyesha watoto wao katika muda unaotakiwa.
Hakuna ubishi kwamba mazingira ya ajira ndiyo yamechangia watoto wake pacha kunyonya kwa muda mfupi kabla ya kukataa wenyewe wakiwa na umri wa miezi sita. Ingawa wapo akina mama wengine ambao inadaiwa kutokana na sababu binafsi, hukataa kuwanyonyesha watoto wao, kwa Shukuru ni tofauti. Alitamani kuwanyonyesha watoto wake kila siku na kwa muda mrefu.
Ukamuaji maziwa
Hata hivyo, laiti Shukuru angezingatia utaratibu wa kukamua maziwa na kuyaacha nyumbani kwa ajili ya kuwalisha watoto wake, pengine asingekumbana na tatizo la watoto kukataa maziwa ya mama, maziwa ambayo yangekuwa mchango mkubwa katika afya zao, mintarafu suala zima la kujenga akili zao na ukuaji wa mwili. Wataalamu wanasema kwamba ukamuaji maziwa ni njia ambayo inaweza kuwasaidia akinamama walioko maofisini au kwenye shughuli za biashara kuwahakikishia watoto wao maziwa yao pale wanapokuwa hawako nyumbani.
Wanasema maziwa ya mama yakikamuliwa na kuwekwa kwenye chombo kisafi yanaweza kukaa kwa muda wa saa 8 bila kuharibika na yakiwekwa kwenye jokofu huweza kukaa zaidi ya saa 36. Hakuna utafiti umefanyika kwa watoto pacha wa Shukuru kujua kama wana tatizo la udumavu au la, lakini kutonyonyesha vizuri watoto hadi kufikia umri wa miaka miwili au zaidi kunatajwa pia kuwa chanzo cha udumavu.
Udumavu ni hali ya watoto kutokua kimwili na kiakili hadi kiwango kinachotakiwa kutokana na lishe duni yakiwemo maziwa ya mama na hili huanzia wanapokuwa tumboni mwa mama zao. Kwa mujibu wa Jukwaa la Lishe nchini (Panita), udumavu mara nyingi hutokea ndani ya siku 1,000 za mtoto zinazohesabiwa tangu mimba kutungwa hadi mtoto anapofikisha umri wa miaka miwili kamili.
“Siku hizi 1,000 zikizingatiwa na wazazi kwa maana ya lishe bora kwa mama na mtoto akishazaliwa kwa kumnyonyesha ipasavyo hadi kuadhimisha miaka miwili ya kuzaliwa kwake, hupunguza pia uwezekano wa magonjwa ya muda mrefu na mzio (allergy),” anasema Jane Msagati, Mtaalamu wa Lishe wa Panita. Anasema mtoto akishakuwa na udumavu, ni tatizo lisilorekebishika maisha yake yote na kwamba hata kama ukimwangalia kwa umbo ukaona hana tofauti na wengine, lakini huwa nyuma kwa kila kitu kulinganisha wenzake hususani kwenye masomo darasani.
Jane anatoa takwimu za mwaka jana zinazoonesha kwamba watoto milioni 2.5 wa Tanzania, sawa na asilimia 34 ya watoto wote walipata udumavu. Takwimu zingine zilizotolewa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto zinaonesha kwamba Mkoa wa Rukwa, ndio unaoongoza kwa udumavu, ukiwa na asilimia 56.6 ya watoto wenye tatizo hilo ukifuatiwa na Ruvuma yenye asilimia 44.4, Kagera yenye asilimia 41.7 na Iringa yenye asilimia 41.6.
Sababu zaidi watoto kukataa kunyonya
Kama tulivyoona kwa kisa cha Shukuru kwamba watoto wanaweza kukataa kunyonya kutokana na mama kuchelewa kuwanyonyesha kutokana na ajira, mtoto anaweza pia kukataa maziwa kutokana na kile anachokula mama na kusababisha maziwa kuwa na harufu au ladha tofauti. Jane wa Panita anasema endapo mama atakuwa anakunywa pombe wakati ananyonyesha, kuna uwezekano wa maziwa kuwa na harufu ya pombe kiasi cha kumfanya mtoto kuyakataa.
Anasema maziwa yanaweza pia kuwa na harufu kutegemea dawa alizotumia mama kutibu maradhi fulani. “Ndio maana mama anayenyonyesha anapopata maradhi, lazima dawa anazotakiwa kunywa ziwe ambazo zinaruhusiwa kwa mama anayenyonyesha vingine zinaweza kumwathiri mtoto ikiwemo hiyo ya kusababisha maziwa yake kuwa na harufu au ladha itakayomfanya ayachukie,” anasema Jane.
Machapisho kadhaa yanaonesha kwamba kama mama hamweki vizuri mtoto wakati wa kunyonya kinaweza kuwa pia chanzo cha mtoto kukataa kunyonya. Kusaidia akinana mama walio kwenye ajira Kama tulivyosikia kisa cha Shukuru, ajira ilichangia sana kuwafanya wanawe kukataa kunyonya. Ili kuwasaidia akina mama kama Shukuru kumekuwa na mapendekezo ya aina mbili, moja likiwa ni kuongeza muda wa likizo ya uzazi.
Wakati dunia inaadhimisha wiki ya unyonyeshaji watoto , umefika wakati sheria za kazi ziangaliwe; ikiwezekana, mama apate likizo ya uzazi kwa zaidi ya miezi sita au hata mwaka. Ingawa kwa sasa akina mama wanaonyonyesha huruhusiwa kuondoka kazini mapema, lakini kwa jiji kama la Dar es Salaam ambalo lina tatizo kubwa la usafiri na foleni, wengi wanalalamika kwamba bado wanachelewa kufika nyumbani na hivyo kutowanyonyesha watoto wao kwa muda mwafaka.
Pendekezo lingine linalotolewa ni waajiri kutenga vyumba maalumu kwa ajili ya kunyonyeshea, ambavyo vitawawezesha watumishi waliojifungua kuja na watoto wao mafisini baada ya kumalizika kwa likizo ya uzazi.
Katika pendekezo hili ambalo baadhi ya ofisi katika nchi jirani ya Kenya zimeshalifanyia kazi, vyumba vinavyotengwa vinatakiwa kuwa na vifaa maalum kwa ajili ya watoto kama vile vitanda vya watoto, majokofu, jiko na vifaa vya kucheza. Sambamba na hilo, waajiri wanatakiwa pia kuajiri yaya mmoja au zaidi kwa ajili ya kulea watoto wa watumishi. Ni kwa njia hiyo mama anaweza akawa mara kwa mara anatoka kwenda kunyonyesha mtoto wake katika mazingira ya kazini na kurejea kuendelea kuchapa kazi.
Share And Comment Bellow On What You Think About This Post!!!

Comments

Facebook Twitter Youtube